Wednesday 4 March 2015

TMA UKAME KUKABILI NCHI

HALI ya ukame inatarajiwa kukabili nchi kutokana na upungufu wa mvua utakaoathiri pia upatikanaji wa nishati ya umeme. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imehadharisha juu ya hali hiyo na kutaka mamlaka zinazohusika na masuala ya umeme, kuanza kuchukua njia mbadala wa uzalishaji nishati kutokana na tishio hilo.

Aidha, upungufu wa unyevu ardhini kutokana na vipindi vya ukosefu wa mvua, umetajwa kuwa utaathiri shughuli za kilimo katika maeneo mengi nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Agnes Kijazi alitoa taarifa hiyo jana wakati wa kutoa mwelekeo wa mvua za masika kwa kipindi cha Machi, Aprili na Mei mwaka huu.

Alisema kwa kipindi hicho, mvua haitarajiwi kuwa ya kuridhisha katika maeneo mengi ya nchi. Alisema mvua za wastani na juu ya wastani, zinatarajiwa katika baadhi ya maeneo hususan Kanda ya Ziwa Victoria na maeneo ya kusini mwa nchi.

Mvua zitaanza mapema katika maeneo ya Kanda ya Ziwa Victoria na baadhi ya maeneo ya ukanda wa Pwani ya Kaskazini. "Pamoja na kuwapo kwa uwezekano wa matukio ya mvua kubwa katika maeneo yanayotarajia kupata mvua juu ya wastani, hali hiyo pia inaweza kujitokeza katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani," alisema Kijazi.

Maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua, mvua zinatarajia kuanza mapema na pia kuwapo kwa vipindi vifupi vya ukame katika maeneo mengi hususani Machi na Mei.

Mvua zilianza wiki ya nne ya Februari katika mikoa ya Kagera, Geita, Mara na Mwanza, huku kanda hiyo ya Ziwa ikitarajia kupata mvua za wastani na juu ya wastani. Kwa upande wa Mikoa ya Simiyu na Shinyanga, inatarajiwa kuwa na mvua za chini ya wastani.

0 comments