Wednesday 6 April 2016

RAISI MAGUFULI KUVUKA MIPAKA KWA MARA YA KWANZA

By    

RAIS John Magufuli leo atafanya ziara yake ya kwanza nje ya nchi baada ya kukaa nchini siku zote tangu ashike madaraka ya kuiongoza Tanzania Novemba 5, mwaka jana kwa kuzuru Rwanda.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje Ushirikiano wa Kikanda na Kimataifa, Rais Magufuli atatoka kwa mara ya kwanza nje ya anga ya Tanzania baada ya siku 151 kwa mwaliko wa Rais Paul Kagame wa Rwanda.

Taarifa hiyo ilisema Dk Magufuli atakuwa na ziara ya siku mbili ya kikazi katika nchi hiyo mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na ambayo pia ni mshirika wa karibu wa Tanzania.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, wakati wa ziara hiyo, Rais Magufuli na mwenyeji wake Rais Kagame wanatarajiwa kuzindua Daraja la Kimataifa la Rusumo pamoja na Kituo cha Pamoja cha Forodha (OSBP) ambacho ni kituo muhimu chini ya mwavuli wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Kituo hicho katika mpaka wa Tanzania na Rwanda, siyo tu muhimu katika kurahisisha mwingiliano kati ya nchi hizo mbili, lakini pia kitaboresha uhusiano na matumizi ya Rwanda katika Bandari ya Dar es Salaam.

Baada ya sherehe za uzinduzi, viongozi hao wawili watakwenda mjini Kigali ambako watafanya mazungumzo kuhusu uhusiano kati ya nchi hizo mbili na pamoja wataweka shada la maua kwenye Kumbukumbu ya Mauaji ya Kimbari mjini Kigali ikiwa ni kukumbuka mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka 1994.

Ikiwa ni safari yake ya kwanza nje ya nchi tangu achaguliwe Oktoba 25, mwaka jana, ziara hiyo ni kielelezo cha jinsi Tanzania inavyoimarisha uhusiano wake na majirani zake.

Akiwa Mwenyekiti wa EAC, ziara hii ya kwanza nje ya nchi ya Rais Magufuli akiifanya katika ukanda huo, pia inaonesha msimamo wake wa kisiasa katika kuimarisha mchakato wa utengamano na mahusiano kati ya nchi wanachama wa EAC.

Katika hatua nyingine, vyombo vya habari vya Rwanda mbali na kueleza kuwa Tanzania ni mshirika mkubwa wa nchi yao kiuchumi, ikiwa inatumia Bandari ya Dar es Salaam kusafirisha na kupokea shehena ya asilimia 60, pia wananchi wake ni watu wanaoshirikiana kijamii.

Vilieleza kuwa mbali ya wananchi hao wa Rwanda, baadhi yao kuishi Tanzania, lakini wanaiona kuwa ni kama makazi yao ya pili. Aidha, vilisema kuwa Rais Kagame ameeleza kuvutiwa kwake na Rais Magufuli hasa msimamo wake katika kukabiliana na rushwa.

Chanzo: Habari Leo

0 comments