Monday 18 December 2017

MASHIRIKA 40 YAUNGANA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA MASOKONI JIJINI DAR ES SALAAM

 Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Equality fo Growth (EfG), Jane Magigita (kulia), akizungumza na wadau wa kupinga ukatili wa kijinsia katika mkutano wa pamoja uliofanyika mwishoni mwa wiki Hoteli ya Lamada jijini Dar es Salaam.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Pugu Poverty Alleviation and Development Agency (PPADA), Abraham Silumbu, akitoa taarifa ya utafiti walioufanya katika Soko la Tandale na Magomeni.
 Wadau wakiwa kwenye mkutano huo.
 Ofisa Ufutiliaji na Tathmini wa Shirika la Eguality for Growth (EfG), Shabani Lulimbeye, akitoa mada kwenye mkutano huo.
 Mkutano ukiendelea.
 Wadau wakisikiliza mada 
 Mkurugenzi wa Shirika la Esscreative and Legal Foundation, Erick Mukiza akimuelekeza jambo Mwanasheria mwenzake, Mchala Hamisi kwenye mkutano huo.
 Mkurugenzi wa Shirika la Wodevota, Catherine Mhagama kutoka mkoani Ruvuma akichangia jambo kwenye mkutano huo.
 Mkurugenzi wa Shirika la Nurget Development in Tanzania (NDT), Hemed Ngochele akichangia jambo. Kushoto ni Mwakilishi kutoka Chama cha Waandishi Wanawake Tanzania (Tamwa), Neema Bishubo.
 Mratibu wa Mradi wa Mpe Riziki si Matusi wa EfG, Susan Sita, akiwa katika mkutano huo.
Mratibu wa Programu wa Shirika la Tanzania Network of Women, Kennedy Godwin akichangia jambo.

Na Dotto Mwaibale

Mashirika 40 yasiyo ya kiserikali yameungana na Shirika la Equality for Growth (EfG) katika kukabiliana na ukatiti wa kijinsia masokoni dhidi ya wanawake.

Akizungumza mwishoni mwa wiki kwenye mkutano wa wadau kutoka katika mashirika hayo, Mratibu wa Mradi wa Mpe Riziki si Matusi wa EfG, Susan Sita alisema shirika hilo liliona ni vizuri kupanua wigo wa kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia masokoni kwa kuyashirikisha mashirika mengine.

"Tuliona ni vizuri kuyashirikisha mashirika mengine katika mapambano haya ambapo mashirika 40 kutoka Manispaa za Temeke, Ilala na Kinondoni yalikubali kati ya hayo manne yameanza kufanya kazi hiyo rasmi kwenye masoko ya Magomeni na Tandale wilayani Kinondoni," alisema Sita.

Aliongeza kuwa, mkutano huo malengo yake ni kuelezea mradi wa mfano kwa wadau na mashirika mbalimbali yanayojihusisha na masuaya la utoaji haki ili kupanua wigo wa utoaji wa taarifa juu ya vitendo vya ukatili vinavyofanyika kwenye masoko.

Alitaja malengo mengine ni kuona mashirika mengine yanavyoweza kutumia mradi wa mfano wa sokoni na kuusambaza katika masoko mengine Tanzania ikiwa ni pamoja na kuandaa mikakati ya pamoja na namna ya kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia kwenye masoko.

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo, Jane Magigita alisema ushirikishaji wa mashirika hayo ulianza mwaka 2015 na kazi kubwa ya mashirika hayo ni kuwakomboa wanawake masokoni kwa kupinga ukatili wa kijinsia.

Alitaja kazi nyingine ni kuboresha uhusiano kati ya wanawake wafanyabiashara na maofisa wa masoko katika kujenga uwajibikaji pamoja na kuona wanawake wafanyabiashara wa Manispaa ya Ilala, Temeke na Kinondoni wanafanya shughuli zao kwenye mazingira huru dhidi ya ukatili wa kingono, kiuchumi, kimwili, matusi na  kisiasa huku wakipewa heshima kama binadamu wengine na kujipatia kipato chao bila ya vikwazo.

"Tunahitaji kuona tunafanikisha ushirikiano kati ya watekeleza sheria, kamati za masoko, viongozi na maofisa wa Manispaa,  Polisi na wafanyabiashara wote katika kudhibiti ukatili wa wanawake katika masoko," alisema Magigita.

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Pugu Poverty Alleviation and Development Agency (PPADA), Abraham Silumbu alisema ushirikiano huo umewapa mori wa kazi kwani utasaidia kupunguza vitendo hivyo vya kikatili masokoni nchini.

"Kwa kweli tumeanza kuona matunda ya ushirikiano huu tumepanga mapambano haya kuyapeleka katika masoko yote hapa nchini," alisema Silumbu. 


0 comments