Saturday 3 March 2018

LINAH : SIHITAJI KUOLEWA


MWANAMUZIKI wa Bongo fleva, Linah Sanga amesema hana mpango wa kuolewa licha ya kuzaa mtoto na mwanaume anayeitwa Shabani au Director Ghost.

Lina ambaye amerudi kwenye muziki hivi karibuni na kutoa wimbo wake mpya unaoitwa ‘Same boy’ aliomshirikisha msanii mwenzake Rachel Kizunguzungu amesema, ndoa ni kitu nyeti hawezi kukurupuka.

“Ndoa ni kitu nyeti sana siwezi kukisema tu napenda na ninatamani kuolewa mimi ni mtoto wa kike lakini sidhani kama niko tayari kwa sasa hivi kuolewa yaani Mungu atusamehe tu tunazaa nje ya ndoa sawa lakini suala la ndoa ni la kujipanga,” amesema Linah.

Pia alisema baba mtoto wake yuko tayari waoane lakini yeye ndio hayupo tayari ingawa alisema kuna mambo yao yanaowafanya wasioane ambayo wanayajua wenyewe. Kumekuwa na tetesi kuwa wawili hao hawawezi kufunga ndoa kutokana na tofauti za kidini ambapo Linah ni mkristo lakini mpenzi wake ni muislamu.

Linah alikuwa amepumzika kufanya muziki kwa kipindi kirefu baada ya kuwa mjamzito mwaka jana na kujifungua mtoto wa kike aitwaye Tracey.

0 comments