Friday 9 March 2018

TUZO KWA WAANDISHI WA HABARI ZA MAJI ZATANGAZWA TENA

By    



Shirika lisilo la kiserikali la Shahidi wa Maji kwa kushirikiana na wadau mbalimbali nchini na ne ya Tanzania kupitia programu yake ya Uhakika wa Maji, imetangaza kuongezwa muda wa uwasilishwaji wa machapisho na programu za redio na runinga kutoka kwa waandishi na vyombo vya habari ili kuwania tuzo za uandishi wa habari za maji.


Tuzo hizi, zilizinduliwa  na Shahidi wa Maji pamoja na washirika wake kwa mara ya kwanza mwezi Juni mwaka 2017, na kupewa jina la ‘Tuzo za Habari za Maji. Ili kushiriki katika tuzo hizi, waandishi watapaswa kuwasilisha kazi zao walizochapisha au walizorusha katika vyombo mbalimbali vya habari zinazohusu masuala mtambuka ya maji kama vile; usimamizi na utawala wa rasilimali maji, ukame, mafuriko, usambazaji maji, uchafuzi wa mito na vyanzo vya maji na kadhalika.


Vyombo vya habari pamoja na waandishi watakaoshinda tuzo hizi watapata zawadi mbalimbali ikiwemo fedha taslimu, vifaa vya kuboresha ufanisi wa kazi kama vile kamera na kompyuta mpakato, kombe la tuzo pamoja na vyeti vya ushiriki, hii ikiwa na lengo la kuboresha uwajibikaji miongoni wa wadau wa sekta ya habari katika kuchapa na kusambaza habari zihusuzo maji ili kuleta mabadiliko chanya, endelevu na ya kudumu katika sekta ya maji na kuleta hali ya usalama na uhakika wa maji kwa watanzania wote.


Pia, makala/kazi a za washindi   zitapata fursa ya kurushwa kwenye tovuti zetu na kusambazwa katika vyomba mbalimbali vya habari na mitandao ya kimataifa kama vile: BBC, UK Guardian, Circle of Blue and Ooska News ambayo ni nafasi na fursa ya kipekee kwa waandishi na vyombo vya habari kusomwa zaidi na kutambuliwa kwa mchango wao katika kusaidia kuboresha sekta ya maji nchini.
Tuzo hizi zimeandaliwa mahsusi kwa waandishi na vyombo vya habari ambavyo vinatoa taarifa za masuala ya maji, kuchochea mabadiliko chanya katika uwajibikaji wa wadau wa sekta ya maji.  Shahidi wa Maji na washirika wake imejikita katika kufanya kazi kubadilisha namna ambavyo rasilimali maji inasimamiwa kwa manufaa ya wananchi wote, mazingira na uchumi wa nchi. Aidha, ili kufanikisha hayo shirika hilo na washirika wake wanafanya kazi kwa namna mbalimbali kama vile; Kusaidia jamii zenye uhitaji kuweza kutambua haki na wajibu walionao katika kuwezesha utekelezaji wa sheria zilizopo na kuwezesha jamii kufuatilia utatuzi wa matatizo ya usalama wa maji katika maeneo yao kwa watoa huduma ikiwemo serikali na sekta binafsi.


Mwisho wa uwasilishaji wa kazi za waandishi na vyombo vya habari umetajwa kuwa tarehe 31 mwezi Mei mwaka 2018. Kufahamu zaidi kuhusu namna ya ushiriki na kupakua chapisho la maelekezo, vigezo na masharti tafadhali tembelea http://www.shahidiwamaji.org au tuma baruapepe kwenda kennedymmari@shahidiwamaji.org

0 comments