Friday 9 March 2018

WAKURUGENZI WA HALMASHAURI MKOANI GEITA WAKUMBUSHWA KUTENGA FEDHA KWA AJILI YA WABAWAKE

By    
Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe Robert Gabriel akisisitiza umuhimu wa kuheshimu wanawake wakati akihutubia wananchi waliojitokeza kwenye maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani yanayoadhimishwa kimkoa katika Wilaya ya Bukombe Mkoani humo, Jana 8 Machi 2018. Picha Zote Na Mathias Canal-Wazo Huru Blog
Baadhi ya wanawake Wilayani Bukombe wakifatilia maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani yanayoadhimishwa kimkoa katika Wilaya hiyo Mkoani humo, Jana 8 Machi 2018.
Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe Robert Gabriel akiongoza zoezi la ukataji keki kabla ya kuhutubia wananchi waliojitokeza kwenye maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani yanayoadhimishwa kimkoa katika Wilaya ya Bukombe Mkoni humo, Jana 8 Machi 2018.
Mbnge wa Jimbo la Bukombe ambaye pia ni Naibu Waziri wa madini Mhe Doto Mashaka Biteko akichangia shilingi 500,000 kuunga mkono harambee iliyoendeshwa na Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe Robert Gabriel ambaye naye alichangia shilingi laki tano kwa ajili ya jukwaa la wanawake Jimbo la Bukombe

Na Mathias Canal, Geita

Wakurugenzi wa Halamshauri za Wilaya katika Mkoa wa Geita wamekumbushwa kutekeleza wajibu wao kwa kutenga fedha asilimia 4 kwa ajili ya mfuko wa maendeleo ya wanawake, asilimia 4 kwa ajili ya mfuko wa maendeleo ya vijana na asilimia 2 kwa ajili ya watu kwenye ulemavu.

Wakurugenzi hao wametakiwa kuongeza kasi katika kuendelea kuchambua na kutambua vikundi vya wanawake na vijana vyenye mwelekeo wa kuzalisha Mali ghafi kwa ajili ya kulisha viwanda vidogo na vya kati ili kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe Robert Gabriel wakati akihutubia wananchi waliojitokeza kwenye maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani yanayoadhimishwa kimkoa katika Wilaya ya Bukombe.

Alisisitiza kuwa vikundi hivyo vinapaswa kujengewa uwezo wa kifedha, mafunzo pamoja na vifaa na hatimaye viweze kuchangia katika azma ya Serikali ya Tanzania ya uchumi wa viwanda kwani kupitia fursa hizo wanawake wengi watajiajiri na kuajiri watu wengine katika sekta isiyo rasmi.

Alisema kuwa sambamba na kuwajengea uwezo wanawake lipo jukumu la kuwalinda wanawake hao pamoja na wasichana dhidi ya vitendo vya ukatili kimwili kama vipigo, ubakwaji, ndoa za utotoni na kuwarubuni kimapanzi wabinti wadogo.

Aidha, amezitaka mamlaka zote ndani ya Mkoa wa Geita kuhakikisha zinatoa ushirikiano kwa wajumbe wa kamati zinazoundwa katika ngazi zote ili kwa pamoja kuhakikisha vitendo vyote vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto vinatokomezwa.

Katika hatua nyingine Mhe Gabriel amezitaka Halmashauri za Wilaya kushirikiana na wadau mbalimbali kutenga bajeti na kuendelea kuweka mipango shirikishi ya kusaidia kutatua changamoto zinazowakabili wanawake na wasichana ikiwa ni pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu na usalama wa mtoto wa kike na kulinda mustakabali wake kwa kumuwezesha kiuchumi, kielimu, kiafya na kumlinda dhidi ya vitendo vya ukatili kimwili.

Alisema kuwa kauli mbiu ya Kitaifa kwa mwaka huu ni "KUELEKEA UCHUMI WA VIWANDA: TUIMARISHE USAWA WA KIJINSIA NA UWEZESHAJI WANAWAKE VIJIJINI" imeakisi dira ya Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe. Dkt John Pombe Magufuli kwa muktadha wa kuhakikisha Tanzania inakuwa ni nchi ya uchumi wa viwanda.

Alisema Serikali inatambua nguvu na ufanisi wa wanawake kwani kupitia vikundi vya kiuchumi, VICOBA, SACCOS na vikundi vya kijamii wamekuwa wakijihusisha na shughuli mbalimbali za kiuchumi; Uchakataji wa malighafi ili kuongeza thamani, biashara ndogondogo, ufugaji ushonaji nguo, kilimo cha mazao, bustani za mbogamboga na matunda na nyinginezo.

Katika maadhimisho hayo Mbunge wa Jimbo la Bukombe Mhe Doto Mashaka Biteko amewapongeza wanawake Duniani kote kwa maadhimisho hayo ya siku muhimu kwao huku akiahidi kuongeza ushirikiano kupitia vikundi vya mbalimbali ambavyo ni msingi wa ustawi na uimara wa Jumbo hilo na Taifa kwa ujumla wake.

Sambamba na hayo pia Mhe Biteko amechangia shilingi laki tano (500,000) kwa kuunga mkono harambee iliyoendeshwa na Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe Robert Gabriel ambaye naye alichangia shilingi laki tano kwa ajili ya jukwaa la wanawake Jimbo la Bukombe.

MWISHO.

0 comments