Sunday 1 December 2013

AZAM MEDIA KUJA NA AZAM FM, AZAM TV HEWANI DES 06


   azam tv

KAMPUNI ya Azam Media imezindua rasmi kituo cha televisheni ya Azam TV ‘Burudani kwa Wote’ ambacho kitaanza kuwa hewani kuanzia Desemba 6, mwaka huu.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Azam Media, Rhys Torrington, alisema matangazo hayo yatakuwa yakipatikana Tanzania nzima na nchi nyingine za Afrika Mashariki kwa kutoa burudani na vipindi mbalimbali.

Alisema kituo hicho kitakuwa na huduma kutoka chaneli 50 zikiwemo za kimataifa, za ndani ya Tanzania na tatu kutoka Azam zitakazorusha matangazo ya Kiswahili, kimataifa na filamu za Kitanzania.

“Kwa kutazama michezo, sinema na matangazo mbalimbali ya miundo ya maisha mteja wetu atakuwa akilipia sh 12,500 kwa mwezi ili kupata matangazo yetu kwa ubora na muonekano mzuri,” alisema Torrington.
Torrington alisema kituo hicho kitakuwa kikirusha moja kwa moja Ligi Kuu ya Bara kupitia chaneli maalumu na kuandaa vipindi mbalimbali kupitia watayarishaji wake.

Aliongeza kuwa Azam Media iko mbioni kuanzisha kituo cha radio cha Azam FM.

Naye mgeni rasmi katika uzinduzi wa kituo hicho, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, mbali ya kuipongeza familia ya Bakhressa kuwekeza katika teknolojia ya utangazaji, alisema hatua hiyo inadhihirisha Tanzania kuwa mstari wa mbele Afrika katika mabadiliko ya urushaji wa matangazo ya televisheni kutoka analojia kwenda dijitali kwa haraka.

Makamba alisema serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa Azam Media na kuzidi kubuni sera nzuri zitakazoongeza uwekezaji katika sekta ya utangazaji.

Aidha, alitoa changamoto kwa vijana wa Kitanzania wenye vipaji, kuitumia fursa ya Azam TV kuandaa programu zao na kujiongezea kipato badala ya kukaa kulaumu na kutuhumu.


CHANZO: TANZANIA DAIMA

0 comments