Saturday, 8 February 2014

Wasaka ajira ugenini kuweni makini-IOM

Shirika la Kimataifa la Wahamiaji (IOM), limewaonya watu wanaopenda kwenda kufanya kazi katika nchi nyingine, dhidi ya ongezeko la mashirika yanayosafirisha binadamu kwa kivuli cha kutoa misaada ya kibinadamu.

Tayari shirika hilo limetoa orodha ya mashirika 23 bandia 23, yanayojitangaza kuwa yanawatafutia watu kazi katika mabara ya Ulaya, Asia na Marekani.

Kwa mujibu wa taarifa za shirika hilo, imebainika kuwa watu hao wanaopata kazi wanaishia katika kunyanyaswa.

Msemaji wa shirika hilo hapa nchini, Husna Tandika aliliambia gazeti hili hivi karibuni kuwa baadhi ya Watanzania wameshanaswa katika mtego wa mashirika hayo, yanayotumia mitandao ya kijamii kujitangaza.
Alisema watu wengi wamekuwa wakiingizwa katika biashara hiyo kwa sababu ya tamaa ya kutaka kwenda nje ya nchi na kupata kipato kikubwa, ili kuishi maisha bora.

Baadhi ya mashirika yaliyotajwa kujihusisha na mtandao wa biashara hiyo haramu ni pamoja na Shirika la Kusajili Wafanyakazi Australia (AIWR/RP), Muungano wa Taasisi za Kuajiri Wafanyakazi Canada (CAWRA), Shirika la Kuajiri Wafanyakazi wa Kigeni Canada (CFWRPA) na Kituo cha Kimataifa cha Kuajiri Wafanyakazi cha Canada (CIRC).

Katika orodha hiyo pia kuna Chama cha Kimataifa cha Kuajiri Wafanyakazi (CIWRA), Wakala wa kutafuta Wafanyakazi (CRA), Mpango wa Kutafuta Wafanyakazi Canada (CWRP), Kamati ya Misaada ya Wakimbizi (GCRHA) na Mpango wa Kimataifa wa kubadilishana wafanyakazi (GIEP).

Kwa mujibu wa tovuti ya Shirika la kuajili wafanyakazi wa kigeni nchini Canada (CFWRPA), ambalo pia limetajwa kujihusisha na biashara ya kusafirisha binadamu, watu wote watakaotafutiwa kazi na shirika hilo nchini Canada watalipwa mishahara mikubwa na hawatabaguliwa kwa rangi, umri, dini au uraia wao.

Pia, waombaji wanapaswa kuwa na vipaji mbalimbali na wenye uwezo wa kuzungumza lugha moja kati ya Kiingereza, Kifaransa na Kihispania.

Hata hivyo, IOM linaseama kuwa mashirika hayo hudanganya kuwa yanashirikiana na mashirika ya umoja wa mataifa, ili kuwavutia watu wengi, hasa kutoka barani Afrika.




chanzo: Mwananchi

0 comments