Wednesday 8 October 2014

WALIMU WANAOVAA VIMINI, VIMODO KUKIONA

Kutoka Habari leo

HALMASHAURI ya Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma imesema haitawavumilia walimu walevi, pia walimu wa kike wanaovaa mavazi mafupi na yanayoonesha maungo ya miili yao na walimu wa kiume wanaovaa suruali za kubana ‘vimodo’. Kauli hiyo ilitolewa juzi na Ofisa Elimu wa Wilaya ya Bahi, Mary Mathew wakati akizungumza na walimu wapya wa shule za msingi kwenye semina elekezi inayohusu utendaji wa kazi zao.

Alisema ualimu ni kazi inayohitaji nidhamu ya hali ya juu kutokana na walimu kuwa walezi wa watoto wanaokuwa wanawafundisha, kwa hiyo ni vyema wakavaa mavazi ya heshima kutokana na wao kuwa kioo cha jamii.

Alisema ni marufuku kwa walimu kuvaa nguo fupi na zile zinazoonesha maungo ya miili yao.

“Walimu watakiwa kuonesha maadili mema kwani ni mabalozi kwa jamii inayowazunguka pamoja na wanafunzi wanaowafundisha,” alisema .

Alisema hatarajii kuona walimu wanavaa nguo zinazodhalilisha taaluma hata kama wao wanazipenda.

“Hasa ninyi kinadada na hata vijana mkinivalia vimodo, kwa kweli sitowavumilia walimu ndani ya Wilaya hii ya Bahi kwani mnatakiwa kuonyesha mfano kwa jamii na wanafunzi mnaowafundisha,’’ alisema.

Pia aliwataka walimu hao kuzingatia miiko ya kazi kwa mujibu wa waraka na sheria za serikali, ili kuleta ufanisi katika kuboresha elimu.

Alisema walimu wengi wanapopata ajira wamekuwa wakijisahau kama wao ni watumishi wa Serikali na kufanya maamuzi ambayo ni kinyume na waraka na maagizo ya kazi zao.

Naye, Ofisa Utumishi wa Wilaya ya Bahi Fredrick Kayombo amewashauri walimu hao kutumia fursa zao katika kuanzisha miradi itakayowafanya wakopesheke kwenye taasisi za kifedha.

Pia aliwataka hao wanapokuwa kwenye vituo vyao vya kazi kujihadhari na matumizi ya muda wa kazi pindi wanapokuwa kazini.

“Kamwe hatutawavumilia walimu watakaobainika kutumia muda huo wa kazi kwa unywaji wa pombe,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bahi, Rachel Chuwa alisema wilaya hiyo imepata walimu wapya zaidi ya 70 na utaratibu wa mafunzo elezi kwa walimu wapya una lengo la kuwaondolea woga na hofu walimu ili waweze kufanya kazi zao vizuri.

Alisema mwaka jana wilaya hiyo ilishika nafasi ya tano kati ya saba kwa ufaulu mkoani Dodoma na anatumaini walimu hao watasaidia kuongeza kiwango cha ufaulu kutokana na kuonesha ari ya kufanya kazi.

“Nitasikia amani kubwa kama mtaipandisha Bahi na kuwa nafasi ya juu,” alisema.

Pia aliwataka walimu hao kutulia kwenye vituo vyao vya kazi kutokana na baadhi ya walimu kuanza kuomba uhamisho kwa kisingizio cha ndoa.

“Kila kitu kina utaratibu wake kumbuka umeshaingia kwenye ndoa na Serikali kwenye hilo tutaangalia ya kisheria na yale ya kimahusiano hata masuala ya ugonjwa yataangaliwa lazima tuheshimu sheria, kanuni na utaratibu wa kufanya kazi,” alisema.

0 comments