Kutoka Habari leo
HALMASHAURI ya Wilaya ya Bahi mkoani
Dodoma imesema haitawavumilia walimu walevi, pia walimu wa kike wanaovaa
mavazi mafupi na yanayoonesha maungo ya miili yao na walimu wa kiume
wanaovaa suruali za kubana ‘vimodo’. Kauli hiyo ilitolewa juzi na Ofisa
Elimu wa Wilaya ya Bahi, Mary Mathew wakati akizungumza na walimu wapya
wa shule za msingi kwenye semina elekezi inayohusu utendaji wa kazi zao.
Alisema ualimu ni kazi inayohitaji
nidhamu ya hali ya juu kutokana na walimu kuwa walezi wa watoto
wanaokuwa wanawafundisha, kwa hiyo ni vyema wakavaa mavazi ya heshima
kutokana na wao kuwa kioo cha jamii.
Alisema ni marufuku kwa walimu kuvaa nguo fupi na zile zinazoonesha maungo ya miili yao.
“Walimu watakiwa kuonesha maadili mema
kwani ni mabalozi kwa jamii inayowazunguka pamoja na wanafunzi
wanaowafundisha,” alisema .
Alisema hatarajii kuona walimu wanavaa nguo zinazodhalilisha taaluma hata kama wao wanazipenda.
“Hasa ninyi kinadada na hata vijana
mkinivalia vimodo, kwa kweli sitowavumilia walimu ndani ya Wilaya hii ya
Bahi kwani mnatakiwa kuonyesha mfano kwa jamii na wanafunzi
mnaowafundisha,’’ alisema.
Pia aliwataka walimu hao kuzingatia
miiko ya kazi kwa mujibu wa waraka na sheria za serikali, ili kuleta
ufanisi katika kuboresha elimu.
Alisema walimu wengi wanapopata ajira
wamekuwa wakijisahau kama wao ni watumishi wa Serikali na kufanya
maamuzi ambayo ni kinyume na waraka na maagizo ya kazi zao.
Naye, Ofisa Utumishi wa Wilaya ya Bahi
Fredrick Kayombo amewashauri walimu hao kutumia fursa zao katika
kuanzisha miradi itakayowafanya wakopesheke kwenye taasisi za kifedha.
Pia aliwataka hao wanapokuwa kwenye vituo vyao vya kazi kujihadhari na matumizi ya muda wa kazi pindi wanapokuwa kazini.
“Kamwe hatutawavumilia walimu watakaobainika kutumia muda huo wa kazi kwa unywaji wa pombe,” alisema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa
Halmashauri ya Bahi, Rachel Chuwa alisema wilaya hiyo imepata walimu
wapya zaidi ya 70 na utaratibu wa mafunzo elezi kwa walimu wapya una
lengo la kuwaondolea woga na hofu walimu ili waweze kufanya kazi zao
vizuri.
Alisema mwaka jana wilaya hiyo ilishika
nafasi ya tano kati ya saba kwa ufaulu mkoani Dodoma na anatumaini
walimu hao watasaidia kuongeza kiwango cha ufaulu kutokana na kuonesha
ari ya kufanya kazi.
“Nitasikia amani kubwa kama mtaipandisha Bahi na kuwa nafasi ya juu,” alisema.
Pia aliwataka walimu hao kutulia kwenye
vituo vyao vya kazi kutokana na baadhi ya walimu kuanza kuomba uhamisho
kwa kisingizio cha ndoa.
“Kila kitu kina utaratibu wake kumbuka
umeshaingia kwenye ndoa na Serikali kwenye hilo tutaangalia ya kisheria
na yale ya kimahusiano hata masuala ya ugonjwa yataangaliwa lazima
tuheshimu sheria, kanuni na utaratibu wa kufanya kazi,” alisema.
0 comments