Saturday, 15 February 2014

GOOGLE WAJA NA NJIA MBADALA WAKUPUNGUZA AJALI

Inawezekana kuwa na magari yasiyokuwa na dereva? Kampuni ya mawasiliano ya kompyuta ya Google inasema ndiyo. Magari hayo yapo na yataongozwa kwa kutumia kompyuta pekee, huku yakiwa na uwezo mkubwa wa kuepuka au kutosababisha ajali barabarani.

Wanasayansi wa Google wanaosimamia teknolojia hiyo mpya, wanaamini kwamba madereva wanafanya makosa mengi wawapo barabarani, yakiwepo ya kizembe ama bahati mbaya na ndiyo yanakuwa chanzo cha ajali mbaya barabarani.

Wakati teknolojia ya kompyuta ilipogundulika, wanasayansi walisema wamegundua mbinu ya kufuta makosa ya kibinadamu katika shughuli za hesabu.

Waliamini kuwa kila hesabu 500 afanyazo mtu ambaye ni mtaalamu wa fani hiyo, lazima kuwepo na makosa yasiyopungua mawili. Lakini baada ya kugundua kompyuta, maelfu kwa maelfu ya hesabu yanaweza kufanyika bila makosa.

Makosa hayo ya kibinadamu yanayoweza kufanywa na mtu bila kukusudia, ndiyo yanayoaminika kuweza kufanywa na dereva yeyote akiwa barabarani.

Magari hayo yako je?


Mtaalamu wa kompyuta katika Chuo Kikuu cha Stanford, Profesa Sebastian Thrun, anayesimamia, teknolojia hiyo akisaidiana na mhandisi wa kampuni ya Google, Chris Urmson, wanasema teknolojia hiyo itasaidia kuepusha ajali, foleni na pia kupunguza kiwango cha mafuta yanayopotea kutokana na uendeshaji usiofaa.

Mhandisi Urmson anasema magari hayo hayatakuwa na tofauti kwa kiasi kikubwa na mwonekano au miundo ya magari yaliyopo sasa. Kama haitoshi yana chaguo la ama liendeshwe kwa kompyuta ama na dereva.


Mwonekano wake


Kimwonekano, magari hayo anayaelezea yatatofautiana na mengine, kwa kuwa na kifaa maalumu juu ambacho kinasaidia mawasiliano na kutambua maeneo.

Anasema kwenye mfumo wa kompyuta zitatumika programu mbalimbali kama vile ya 3D, ambayo itasaidia kuliongoza gari kulingana na ramani ya eneo.

“Hii ina maana kwamba magari yote yatakuwa yanatumia ramani ambayo lazima iingizwe kwenye mfumo wake ili itambue barabara itakazopita ili kufika aneo ambalo mhusika ama wahusika wanataka” anasema.

Isitoshe anasema gari hiyo ina vihisi vinavyosaidia kutambua njia ambayo linapaswa kupita, ili lisiingilie njia ya magari mengine. Pia kutambua gari au mtembea kwa miguu anayekatiza mbele yake.

Vihisi hivyo ambavyo viko pande zote za gari; mbele, ubavuni nyuma, chini na juu, vinaweza kulisaidia pia kufahamu eneo la taa zinazooongoza magari na kutambua wakati wa kuruhusiwa kupita.

Ili kuhakikisha kuwa ramani za maeneo husika hazina matatizo, mhandisi huyo anasema Google watapaswa kutumia magari yao kuinakilisha vyema kwenye mfumo ambao utakusanya takwimu mbalimbali za maeneo husika.

Ina maana kwamba ili nchi kama Tanzania iweze kutumia teknolojia ya magari hayo, ni lazima kampuni ya Google ilete wataalamu wake nchini ili kuzisoma barabara ambazo magari hayo yatapita.

Ikitokea barabara ikaongezwa ama kubadilishwa mfumo au muundo wake, basi itabidi na ramani ya gari hilo ibadilishwe ili kuepuka makosa.

Mhandisi Urmson anasema kuwa hata kama itatokea taa za barabara zimeruhusu gari hilo, akipita mtembea kwa miguu kimakosa, gari hilo litambaini na kumuacha apite.

“Iwapo gari jingine la namna hiyo litatokeza ghafla katika makutano ya barabara yasiyoongozwa na taa, gari za mfumo huo zitatambuana, hivyo mojawapo litampisha mwenzake apite kwanza.

Gari hizo, anasema zina uwezo wa kutambua wapi zitembee kwa kasi na wapi zipunguze mwendo. Pia zina uwezo wa kufuatilia magari, watembea kwa miguu na hata vitu vingine vya hatari vilivyopo karibu yake.

“Gari hizo zina uwezo wa kutoa ishara ya kuelekeza magari mengine nini yafanye na hata kuelimisha mengine ambayo yanaonekana yanataka kuvunja sheria,” anasema mhandisi Urmson na kuongeza:

“Hii ni teknolojia ambayo katika siku zijazo itafanya usafiri wa barabarani kuwa rahisi zaidi, wa starehe, haraka na wenye ufanisi.”

Google inaamini ifikapo mwaka 2020, magari mengi yanayoendeshwa kwa kompyuta yatakuwa yanatumika hasa katika nchi zilizoendelea.

Kwa mfano nchini marekani magari hayo yameweza kutembea katika miji yenye msongamano wa magari mengi na kutembea zaidi ya kilomita 300,000 bila kusababisha ajali.

Waanzilishi wa teknolojia hiyo katika kampuni ya Google, ni Larry Page na Sergey Brin.



CHANZO: MWANANCHI

0 comments