Saturday, 15 February 2014

Kampuni yalalamikiwa kwa utapeli

BAADHI ya wakazi wa Kibaha, mkoani Pwani, wanailalamikia Kampuni ya Informal Sector Workers Union ya jijini Dar es Salaam kwa madai ya kuwatapeli sh milioni 8.8.

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, wakazi hao walisema lengo lilikuwa ni kutaka kukopa pikipiki na wengine fedha, lakini hadi sasa zoezi hilo halijafanikiwa na hawaoni dalili za kupata mikopo.

Baadhi ya walalamikaji hao; Loyce Isack, Goodluck Marika na Emmanuel Mhina ambaye ni mchungaji wa Kanisa la Pentekoste lililopo Mwanalugali, walisema mgogoro kati yao na kampuni hiyo utaisha endapo watatimiziwa mahitaji yao.

Walisema Machi mwaka jana walipata taarifa ya kuwepo kwa kampuni hiyo katika ofisi ya CCM Wilaya ya Kibaha Mjini ikitoa mikopo ya fedha na pikipiki na ndipo walipokwenda kujiunga kwa kufuata utaratibu walioelezwa, lakini hadi sasa hakuna mikopo iliyotolewa.

Walieleza moja ya taratibu walizotakiwa kufanya ni kuweka dhamana ya sh 650,000 na 500,000 pamoja na bima ya sh 38,000 ili wapate pikipiki na ya fedha na kwamba marejesho yalikuwa yawe sh 56,500 kila wiki ndani ya miezi sita.

Hata hivyo, pamoja na kufuata taratibu walizopewa pamoja na kutoa fedha hizo, hakuna mkopo wa fedha wala pikipiki walizopata hadi sasa licha ya kuwepo kwa juhudi za kufuatilia haki zao bila mafanikio.

Walisema wameshapeleka malalamiko hayo katika ofisi za Makao Makuu ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani na kufungua jalada la uchunguzi lenye namba RCO/PE/No 8/2013.

Walieleza hawakuwa na wasiwasi kwa kuwa kampuni hiyo ilikuwa ipo ndani ya jengo la CCM, hivyo waliamini ilikuwa na lengo la kuwasaidia wananchi wake.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Dauda Salmin, alitafutwa kupitia simu yake ya kiganjani  na baada ya kupokea na kusikia mwandishi akieleza kuhusiana na jambo hilo alikata simu na kuzima.




CHANZO: TANZANIA DAIMA

0 comments