Thursday, 28 August 2014

UHAKIKI WA MIPAKA: Wananchi Tanzania, Burundi kuanza kutambua maeneo yao.

Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Dokta Jakaya Mrisho Kikwete amesema hatua ya kuhakiki mpaka wa Tanzania na Burundi baina ya nchi hizo mbili, imelenga kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo ya mipakani kutambua maeneo ya nchi zao ili kuwawezesha kufanya shughuli zao kwa amani na utulivu.
Rais Kikwete amesema hayo katika uzinduzi wa awamu ya kwanza ya kazi ya uzinduzi wa mpaka baina ya nchi hizo mbili, na kisha kufuatiwa na mkutano wa hadhara ambao pia umehudhuriwa na Rais wa Burundi Pierre Nkurunzinza, katika kijiji cha Mgikomero wilayani Ngara Mkoani Kagera.

Rais Jakaya Kikwete pamoja na rais wa nchi jirani ya Burundi Pierre Nkurunziza, wamezindua awamu ya kwanza ya kazi ya utambuzi wa mpaka wa Tanzania na Burundi, iliyoainishwa upya baada ya mpaka wa kwanza uliochorwa na wakoloni wa Kiiingereza na Kibelgiji mnamo mwaka 1924.

Katika Mkutano wa hadhara, Rais Kikwete licha ya kuwataka wananchi wa pande mbili za Tanzania na Burundi kulinda mpaka huo, amesema serikali yake itaendelea na kazi ya kuainisha mipaka yake ili kuhakikisha wananchi wa maeneo ya mipakani wanafanya shughuli zao kwa amani na utulivu.

Kwa upande wake Rais wa Burundi Pierre Nkurunzinza ameipongeza serikali ya Tanzania kwa kuendeleza ushirikiano baina ya nchi hizo na kuahidi kuendeleza umoja na mshikamano baina ya wananchi wake.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Profesa ANNA TIBAIJUKA pamoja na mwenzake wa Burundi Jean Claude Nduwayo wameelezea kiini cha nchi hizo kuamua kuainisha mipaka yake.

Baadhi ya Wataalam na wananchi wameelezea changamoto walizokumbana nazo kabla ya zoezi hilo.

Jumla ya kilometa mia nne na hamsini zimetumika kuainisha mpaka kati ya Tanzania na Burundi huku ukigharimu serikali za nchi hizo, zaidi ya shilingi bilioni mbili nukta sita.

0 comments