Kauli hiyo imetolewa na kiongozi wa chama hicho, Zitto Kabwe katika mkutano wake na viongozi wa chama kwa ngazi ya mkoa wa Dar es Salaam jana na kusema kuwa taarifa zinazoenea kuwa chama hicho kitajiunga na Ukawa sio za kweli.
“Hatuwezi kujiunga na Ukawa kwa kuwa CCM na vyama vingine hawana tofauti kwa sera, lakini ACT ni tofauti kwa kuwa inaheshimu miiko ya uongozi na kubwa zaidi chama chetu kinaongozwa na azimio la Tabora,” alisema Kabwe.
Alisema ACT itasimamisha wagombea katika majimbo yote 10 ya mkoa wa Dar es Salaam kuanzia ngazi ya diwani hadi ubunge na wananchi wasiwe na hofu kuwa chama chao kipo imara na makini kwa kufuata taratibu na miiko waliyojiwekea.
Zitto aliongeza kuwa chama cha ACT hakiwezi kuyumbishwa na kelele za vyama vingine wanaokitaka chama kijiunge nao kwa kuwa hakuna chama chenye sera kama za ACT-Wazalendo ambacho kimedhamiria kurejesha misingi ya usawa na utawala bora.
Hivi karibuni kumekuwepo na tetesi kuwa chama cha ACT Wazalendo kipo katika mchakato wa kujiunga na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ili kuongeza nguvu umoja huo katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Chanzo: Habari leo
0 comments