Monday, 13 January 2014

HUJUMA ILIYOFANYWA KATIKA UADISHI WA HISTORIA

Na Muislam WA Jihad kutoka WASIKILIZAJI WA REDIO IMAAN

Tarehe 27 Aprili, 1985 Julius Kambarage Nyerere, sasa akijulikana kama Baba wa Taifa, katika sherehe kubwa katika viwanja vya Ikulu, alitoa jumla ya medali 3979 kwa Watanzania waliochangia katika maendeleo ya taifa. Kati ya wale ambao walipewa medali hizo alikuwa Sheikh Abdallah Chaurembo.

Wazalendo waliotajwa ndani ya kitabu hiki ambao walipigania uhuru wa Tanganyika, hakuna hata mmoja wao aliyekuwa katika orodha ile ya heshima. Baada ya siku chache kupita, Nyerere kama mtu aliyegutuka alimualika Dossa Aziz Ikulu.

Dossa Aziz, wakati wa kudai uhuru wa Tanganyika alikuwa mtu maarufu, mwenye nafasi, na kujiweza sana. Sasa Dossa baada ya miaka kupita hakuwa akifahamika tena na ule umaarufu na utajiri wake ulikuwa umetoweka. Alikuwa akiishi maisha ya kawaida kijijini Mlandege, maili chache nje ya Dar es Salaam. Katika sherehe ya faragha Nyerere alimtunukia medali Dossa Aziz, rafiki yake wa zamani. 295

Ule Mkutano wa Tabora ulikuwa umeacha kovu lake katika historia ya uhuru wa Tanganyika. Huenda kama si yale masharti ya uchaguzi wa kura tatu, historia ya TANU na kwa hakika ile ya ukoloni Tanganyika isingekuwa hivi ilivyo sasa. Yamkini kusingekuwepo na mgawanyiko katika TANU wala Zuberi Mtemvu asingeunda ANC, na Mashado Plantan - AMNUT; wala suala la udini katika siasa za Tanganyika lisingewekwa katika agenda, jambo ambalo kwa miongo mitatu baada ya uhuru ngurumo zake bado zinasikika na zinatishia utengemano na uthabiti wa nchi. Waislam wanamlaumu Nyerere na Wakristo waliokabidhiwa madaraka ya kutawala nchi kwa msaada mkubwa wa Waislam. Waislam wanadai kuwa wamesalitiwa. Kwa hivi sasa Waislam wako katika mwelekeo wa kujitambua kwa mara ya pili na historia yao yenye mengi sana. Wanaamini majibu ya baadhi ya matatizo yao ya hivi sasa yamo katika historia yao ya zamani.

Mjini Dar es Salaam katika msikiti wa Kitumbini hafla husomwa kila mwaka katika mwezi wa Oktoba kumkumbuka Abdulwahid Kleist Sykes. Hii ni hafla ya kifamilia ikihudhuriwa hasa na wana-ndugu. Ukiachia mbali ule wajibu wa Waislam kurehemiana kama ilivyo kawaida katika Uislam, Abdulwahid hufanyiwa hafla hii pale msikitini kwa sababu nyingine.

Katika umri wake mfupi, Abdulwahid alikuwa akiswali pale msikitini na katika msikiti ule ndipo aliposwaliwa swala yake ya mwisho kabla ya kupelekwa kuzikwa. Abdulwahid alikuwa mtu mashuhuri katika jamii ya Waislam Dar es Salaam. Alifanya shughuli nyingi chini ya Al Jamiatul Islamiyya. Halikadhalika alikuwa katibu baadae rais wa TAA. Ingawa historia ya Tanzania bado haijamtambua mchango wake ni wazi kuwa Abdulwahid ndiye aliyekuwa bongo katika kuasisi TANU chama ambacho kilikuja kuwaunganisha wananchi wa Tanganyika katika kudai uhuru wao kwa Waingereza.

Marika ya Abdulwahid bado wa hai na baadhi yao wanaswali pale msikitini. Huwa wanafurahishwa na kumbukumbu hii ya kumrehemu mwenzao. Karibu walio wengi ni maveterani wa TANU ya miaka ya 1950. Hivi sasa wao ni wazee na kwa uchungu hawana haja na siasa.

Ukiacha ndugu wa marehemu Abdulwahid (sasa hivi wanajumuika na wajukuu zake), marafiki wa karibu na wanachama wa zamani wa TANU, hakuna hata mtu mmoja katika Chama cha Mapinduzi (chama kilichorithi nafasi ya TANU) anaemkumbuka.

Jina la Abdulwahid halitajwi kabisa katika historia ya kudai uhuru wa Tanganyika au katika historia ya kuasisi TANU. Juu ya haya yote Abdulwahid ndiye aliyewasha cheche za kuanzisha harakati za kudai uhuru wa Tanganyika.

Jopo la wana-historia wa Chama Cha Mapinduzi waliopewa jukumu la kutafiti na kuandika historia rasmi ya TANU, hakuna hata sehemu moja waliyotaja jina la Abdulwahid katika kitabu kizima.296 Dhana inayojaribiwa kuenezwa katika kitabu kile ni kuwa kabla ya kutokea kwa Julius Nyerere mwezi Aprili, 1953, alipochaguliwa kuwa rais wa TAA, chama hicho hakikuwa na mwelekeo wowote wa siasa. Kitu cha ajabu ni kuwa kitabu hicho wala hakielezi huo urais wa TAA, Nyerere aliupataje au aliuchukua kutoka kwa kiongozi gani wa wakati ule.

Kitendo hiki kimeondoa hadhi na heshima ya wazalendo wengi waliopigania nchi hii na halikadhalika kimeiondolea TAA heshima ya kuitwa chama cha siasa. Wanahistoria wazalendo pamoja na wanasiasa wa sasa hawataki kabisa kuipa TAA hadhi ya chama cha siasa. Kambona aliiita African Association chama cha majadiliano:

Sasa inakaribia mwaka mmoja toka iundwe Tanganyika African National Union na katika kipindi hiki chama kimekua kikipata nguvu siku hadi siku, wakati mwingine chini ya upinzani mkubwa.

Kama mnavyofahamu chama hiki ni badala ya Tanganyika African Union ambayo ilikuwa sawasawa na chama cha majadiliano.297

Ulotu anaieleza TAA kuwa ilikuwa chama cha ustawi wa jamii.298 Wengine wameieleza TAA kama taasisi ya jamii: Nyerere (1976), halikadhalika Japhet na Seaton (1966).300 TAA wakati mwingine inaelezwa kuwa ilikuwa chama cha vuguvugu za upinzani dhidi ya ukoloni, lakini upinzani wake haukuwa dhahiri: Kaniki (1974), Nyerere (1953) 302 aliieleza TAA kama chama cha vuguvugu la siasa lakini si za dhahiri. Julius Nyerere alipohutubia Baraza la Udhamini la Umoja wa Mataifa, New York, tarehe 7 Machi, 1955 alisema:

Tanganyika African National Union kwa mtazamo mmoja ni chama kipya, lakini kwa mtazamo mwingine ni chama kikongwe. TANU imechukua nafasi ya Tanganyika African Association ambayo ilianzishwa mwaka 1929, kama chama cha kijamii. Tanganyika African National Union, chama kilichochukua nafasi ya African Association miezi kumi iliyopita ni chama kipya kwa maana ni chama cha siasa, wakati TAA ilikuwa chama cha siasa nusunusu.

Wasomi wengine wameishusha TAA kufikia daraja la kuwa klabu: Mwenegoha (1976) anaandika: 'Mwaka 1954, baada ya miaka ishirini na tano ya kutoweza kufanya lolote, Nyerere aliigeuza TAA kutola chama cha kijamii kuwa chama cha siasa chenye kuogopwa kilichoitwa Tanganyika African National Union'. 303

Abdulwahid ambae alitoa mchango wa pekee katika kuunda TANU alikuwa anaiona TAA kama chama cha siasa (1951). 304 Katika kundi la waandishi na wasomi walioandika kuhusu African Association kisha wakabadili mawazo yao kuhusu nini hasa chama kile kilikuwa, ni Nyerere na Hatch ndiyo waliobadili misimamo yao ya awali. Nyerere alipoandika barua kwa Gavana wa Tanganyika, Edward Twining tarehe 10 Agosti, 1953 alieleza kuwa TAA ni chama cha siasa. 305

Lakini baadae alibadili msimamo na kusema kuwa TAA kilikuwa chama cha starehe. Kauli hii ilitawala hotuba za Nyerere na maandishi yake kwa kipindi kirefu. Katika miaka ya hivi karibuni amesikika akisema kuwa TAA kilikuwa 'chama cha siasa kisichokuwa na katiba ya siasa'. Hatch (1976) ameieleza TAA kama chama cha starehe 306 sehemu moja na chama cha siasa sehemu nyingine.307 John Kabudi ameieleza African Association kama 'chama cha watu binafsi wananchi kilichokuwa na mwelekeo wa kitaifa'.308 Ieleweke kuwa hata viongozi wa TAA hawathaminiwi kama wanasiasa. Kaniki, kwa kukosa neno la kuwatambulisha waasisi wa TAA, amewaita wanasiasa na kuwawekea quatation mark:

Nyerere, kabla ya hapo akiwa hajulikani na 'wanasiasa' wengi katika Tanganyika, alikuwa mwalimu katika shule ya Mtakatifu Francis, Pugu, jirani na Dar es Salaam, na alikuwa amechaguliwa rais wa (TAA) mwaka uliopita.309

Kwa mtazamo huo wa Kaniki mzalendo kama Abdulwahid Sykes hakuwa mwanasiasa, ila Nyerere ndiye mwanasiasa. Iliffe (1968)310 alidokeza kuwa historia ya TANU iliyokuwa imeandikwa hadi wakati ule ilikuwa haijakamilika na katika uchambuzi wake alisema kuwa African Association kutokana na mwelekeo na wanachama wake ilikuwa ni chama cha siasa. Kandoro na Japhet, 311 waasisi wa TANU walipata umaarufu wakati Abdulwahid akiwa rais wa TAA mwaka 1952. Hawa walikuwa ndiyo waasisi pekee ambao walifanya kazi na Abdulwahid wakati wa Mgogoro wa Ardhi ya Wameru. Safari ya Kirilo kuja Dar es Salaam na kule kumweka Seaton kama mwanasheria kushughulikia mgogoro ule, kazi yote hiyo ilifanywa na Abdulwahid na uongozi wa TAA wa wakati ule. Ilikuwa Abdulwahid ndiye aliyemhangaikia Kirilo kupata pasi ya kusafiria baada ya kunyimwa pasi kule Arusha. Kirilo na Seaton na halikadhalika Kandoro wamenadika kumbukumbu zao kuhusu ukoloni, lakini cha ajabu na kusikitisha ni kuwa hakuna hata sehemu moja waandishi hawa wametaja mchango wa Abdulwahid hata kwa kuparazia tu. Waandishi hawa wamejaribu kumtumbukiza Nyerere kama kiongozi aliyehusika katika Mgogoro wa Ardhi ya Wameru, wakati yeye hata kuwapo nchini wakati ule hakuwapo. Ukweli ni kuwa wakati mgogoro wa ule ulipofikishwa mbele ya Baraza la Udhamini la Umoja wa Mataifa, New York, Nyerere alikuwa masomoni Chuo Kikuu cha Edinburgh Uskochi akisomea shahada ya pili. Mwandishi aliyejipambanua na hawa wote kwa kutomtaja Abdulwahid ni mama wa Kiingereza Judith Listowel (1965) 312 ambae ingawa amemtaja kijuujuu, ameandika kwenye kitabu chake kuwa Abdulwahid alikuwa mmoja wa waasisi wa TANU.

Katika miaka hii ya karibuni kumejitokeza hamu ya kutaka kuielewa historia ya siasa katika Tanzania na jina la Abdulwahid limekuwa likijitokeza mara kwa mara katika majarida, 313 magazeti, 314 magazeti ya kimataifa, 315 na katika vitabu. 316 Maandiko yote haya yanamtazama Abdulwahid kwa sura tofauti. Yapo yanasema kuwa yeye ndiye alikuwa kinara katika kuunda TANU na kumtia Nyerere katika siasa. Katika maandiko haya Abdulwahid anaelezwa kama mzalendo na mwanamapinduzi. Tandon anamweleza Abdulwahid na wazalendo wengine katika Afrika ya Mashariki kama Chege Kibachia, Makham Singh, Fred Kubai, James Kivu, I.K. Musazi, Erika Fiah na Gama Pinto kama 'viongozi maveterani wa watu wa Afrika ya Mashariki ambao wanahistoria wetu wa sasa wamewasahau'. 317 Wapo waandishi wanaomuona Abdulwahid kama 'kabaila uchwara' kutokana na kuwa alikuwa mtoto wa mfanyabiashara Mwafrika tajiri, Kleist Sykes.

Profesa Shivji anamtuhumu Abdulwahid kwa kushirikiana na wakoloni na anamchukulia kama kabaila uchwara ambae yeye mwenyewe hatoki katika tabaka la wafanyakazi. Akitafakari nafasi ya Abdulwahid kama kiongozi wa makuli katika bandari ya Dar es Salaam wakati wa ukoloni Shivji ansema:

serikali ilipenyeza uongozi wa makabaila uchwara katika chama. Mwezi February 1948 Abdul Sykes, mtoto wa mfanya biashara Mwafrika maarufu, aliombwa na serikali awe katibu wa chama cha makuli. Abdul Sykes hakuwa akifanyakazi bandarini wala hakuwa anatoka katika tabaka la wafanyakazi.318

Hapa Shivji alikuwa anaeleza jinsi Abdulwahid alivyochaguliwa kuwa katibu mkuu wa kwanza katika historia ya vyama vya wafanyakazi Tanganyika. Kwa kutoijua vyema historia ya maisha ya Abdulwahid na vilevile kwa hamaki za misimamo ya mrengo wa kushoto ya Ki-Marx, Shivji ametumia vipimo visivyo sawa katika kumchambua Abdulwahid. Engels anasema bepari uchwara ni 'tabaka la makabaila wa kisasa ambao wanahodhi njia zote za uzalishaji mali za jamii na vilevile wanawaajiri na kuwalipa'.319 Hata hivyo Sklar anasema kuwa dhana hiyo sasa imebadilika kwa hiyo hata ile maana yake ya awali imebadilika:

Hivi sasa neno hilo linatumiwa na wafuasi wa Marx kuieleza tabaka lililo juu katika jamii ambazo zinafuata soko huria na kuachia kuhodhiwa kwa mali kama matokeo ya mali binafsi katika uzalishaji wake.320

Kama Shivji angeliyajua maisha ya Abdulwahid ni wazi kuwa angetumia kipimo kingine kabisa katika kumweleza. Lakini kwa kuwa kilichotumika ni kipimo kisicho sawa, matokeo yake hayakuweza kuwa barabara. Hakuna biashara ya Mwafrika wakati wa ukoloni inaweza kuitwa biashara ya bepari na katika mkumbo wa kujumuishwa katika dhana ya ubepari, kama ubepari ulivyokuwa ukifahamika huko Ulaya. Haya ndiyo matatizo yanayoikumba historia ya Abdulwahid na kwa kweli historia nzima ya taifa la Tanganyika.

Katika wale walioasisi TANU, ni wale tu aliokuwa makao makuu ya TAA ndiyo wanaoweza kueleza historia ya kweli ya chama hiki. Hawa ni John Rupia, Dossa Aziz, Tewa Said Tewa, Julius Nyerere, Dome Budohi, Abdulwahid na Ally Sykes. Hawa ndugu wawili, Abdulwahid na Ally, wao ni baba yao ndiye aliyekuwa muasisi wa African Association akiwa kama katibu wake wa kwanza hapo mwaka wa 1929. Majalada ya akina Sykes kuhusu African Association na TANU yana habari muhimu sana kwa mtafiti kuhusu historia ya ukoloni na juhudi walizofanya waasisi wa taifa la Tanganyika katika kujikomboa. Majalada haya yana habari muhimu na za kutosha kuhusu Nyerere na jinsi alivyopokelewa Dar es Salaam na akina Sykes na jinsi alivyoingizwa katika siasa. Inastaajabisha kuwa kumbukumbu hizi zenye habari muhimu sana kuhusu Nyerere na TANU hazikuguswa kabisa wakati watafiti wa historia ya TANU walipokuwa wakifanya utafiti wao. Inastaajabisha vilevile kuwa, si Ally wala mdogo wake, Abbas ndugu wawili walio hai baada ya kifo cha kaka yao Abdu.

0 comments